Home » Mwalimu Nyerere na Sheikh Kandoro katika uga wa ushairi

Mwalimu Nyerere na Sheikh Kandoro katika uga wa ushairi

by Joshua Kiziba

RAIS wa awamu ya kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere  alizaliwa mwaka 1922 katika  Wilaya ya Butiama Mkoa wa  Mara, mnamo tarehe 14 Oktoba, 1999, aliaga dunia  katika hospitali ya Mtakatifu Thomas jijini London  nchini Uingereza.

Katika uhai wake,  alikuwa ni Mmalenga. Aliandika barua ya Kiserikali kwa mtindo wa utenzi, pia alijibiwa barua hiyo  kwa mtindo wa utenzi na Nguli/Karii,  Hayati Saadani Abdul Kandoro aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo mwaka 1964.

“Huu ni utenzi ulioandikwa kwa njia ya barua iliyotungwa na Muheshimiwa Mtukufu mwalimu J.K. Nyerere,  President wa TANU na Serikali. Aliniletea barua hiyo ili kunizungumza jinsi ya watu wanaopenda kujisaidia katika shughuli za maendeleo na jinsi ya kuwapa moyo dhidi ya adui wa jamii katika shughuli za vijiji.”- Hayati Saadani A. Kandoro

SHEIKH KANDORO, SIKIA!

1. Sheria  husaidia,

Kuijenga Tanzania,

Siyo kazi ya sheria,

     Nchi kutuharibia.

2. Kila nchi ina nia,

Inayoikusudia,

Vile vile ina njia,

   Itakayoipitia.

 3. Tanzania tuna nia,

Ya kujenga ujamia,

Na  njia ya kupitia,

  Ni wote kusaidia.

4. Kijiji cha turadhia,

Kisima kujipatia,

La magambo limelia,

  Watu wakahudhuria.

5. Wakakubali kwa nia,

Kisima kujichimbia,

Aliyewakatalia,

   Kukuye wakamlia.

6. Akenda kushtakia,

Kwa hakimu wa sheria,

Kwamba wamemuonea

    Kuku wake kalmia.

7. Hakimu akasikia,

Akaita jumuia,

Wakaja akawambia,

    Nyinyi wavunja sheria.

8. Basi nawahukumia,

Faini shilingi mia,

 Na sabini za fidia,

    Au jela kuingia.

9. Hakimu wakamwambia,

Itatushinda fidia,

Hata na faini pia,

    Heri jela kuingia.

10. Wakafungwa kwa sheria,

Na maji wakamwachia,

Mwenye kuku kuumia,

     Pamwe na Hakimu pia.

11. Huko ni kusaidia,

Adui wa jumuia,

Nasi kazi ya sheria,

    Ila ya maharamia.

12. Kazi hasa ya sheria,

Kusaidia raia,

Sina nia kuwavunjia,

Wanapojisaidia.

“Huu ni utenzi niliandika kama barua ya kumjibu Mheshimiwa Mtukufu Mwalimu J.K. Nyerere President wa TANU kujibu utenzi wake alioniandikia juu ya wanaoharibu maendeleo ya kijiji katika kazi za jamii.”- Hayati Kandoro.

1. Labeka Mheshimiwa,

Julius msifiwa,

Kambarage muelewa,

    Bwana nakuitikia.

2. Nakuitikia sheria,

Kwamba inasaidia,

Kuijenga Tanzania,

    Na ni nguzo ya Dunia

3. Kutoheshimu sheria,

Huleta wingi udhia,

Amani ikapotea,

     Nchi zikaangamia.

4. Ni msumeno sheria,

Mithali hii natia,

Haitaki kubabia,

    Pendelea liso njia.

5. La mgambo likilia,

Watu wote hudhuria,

Kisima kujichimbia.

     Hilo lataka sheria.

6. Kuna wavivu wa nia,

La mgambo likilia,

Nao anajikalia,

   Huendi kuhudhuria.

7. Mfano huo hatia,

Wengine huufatia,

Na wao hujikalia,

Kazi zetu husinzia.

8. Kimila nimesikia,

Waweza kumsikia,

Kuku wake kujilia,

Lakini sio sheria.

9. Kwa kuwa sio sheria,

Mvivu hujishitakia,

Na walao huumia,

Pia hutozwa fidia.

10. Twazidi kukulilia,

Ifanywe hasa sheria,

By Law kuitia,

Yaweza kusaidia.

11. Yaweza kusaidia,

Kuku tukijilia,

Pasiwepo hata njia,

Mvivu kukimbilia.

12. Kuku tumejilia,

Pasiwe na kuponyea,

Hakimu kumuendea,

Kwamba alipwe fidia.

13. Mkazo twaukazia,

Bila nyuma kurudi,

Twataka kuendelea,

Kuinua Tanzania.

14. Taifa kuitikia,

Kazi kuzishangilia,

Ndilo tunalolilia,

Ndipo tunakazania.

15. Ndipo tuna kazania,

Na tena tuna kania,

Kuishangaza dunia,

Lengo letu kutimia.

16. Bila nguvu kuzitia,

Mkazo wa kisheria,

Unafaa kufatia,

Kazi zitaendelea.

Utii wa Sheria bila kushurutishwa: